Maswali ya mara kwa mara

SACCOS NI NINI NA NI UPI UTOFAUTI NA BENKI

JIBU: Kwa mujibu wa sheria ya vyama vya ushirika na. 6 ya mwaka 2013 sehemu ya kwanza k/f 2.  Na sehemu ya pili k/f 3 (1) neno saccos   ni kifupi cha neno la kiingereza “savings and   credit   co-operative   society” kiswahili likiwa na maana ya chama cha ushirika wa akiba na mikopo.

Huu ni   muunganiko  wa hiari  kisheria,  ambapo   watu  kwa pamoja wakiwa  na  lengo la  pamoja katika  kuanzisha   umoja wao  wa  kifedha,  kwa  lengo la kuweka akiba na kukopeshana  ili  kujikwamua   katika   shughuli zao  za   kiuchumi  na  kijamii   na kugawana ziada iliyopatikana kwa  kufuata sheria , kanuni na taratibu za vyama  vya  ushirika na  mabadiliko  yake.

BENKI: Ni taasisi  ya kifedha   ambayo muundo wake  na taratibu za uendeshwaji wake  ni kwa mujibu wa sheria na 12 ya mabenki na taasisi za kifedha ya mwaka 1991 na mabadiliko yake.  Mtu yeyote anaweza kuwa na akaunti ya benki inayomuwezesha kuweka pesa na kuchukua wakati wowote. Taasisi hizi zinaendeshwa chini ya usimimamizi wa benki kuu na faida yake ni kwa wenye hisa katika benk hizo.

MWANACHAMA ANASHIRIKISHWAJE KWENYE MAAMUZI

JIBU: Katika  uendeshwaji    wa  vyama    vya  ushirika  vya akiba na mikopo kila  mwanachama   anayo haki   sawa  na mwanachama  mwingine, pia  kila  mwanachama  anayo haki  ya  kutoa  maoni  yake  katika  vikao /mikutano  ya  wanachama  ya ngazi ya wilaya, mkoa na mkutano mkuu . URA SACCOS katika  kila  wilaya  kuna  mwakilishi  ambaye  ndiye  anawakilisha  wanachama   katika   mkutano  mkuu kwa kuwasilisha maoni  ya wanachama wa  wilaya  yake, kama ilivyoainishwa katika sheria ya vyama vya Ushirika sehemu ya vi k/f 42, pia katika jedwali la tatu 1 (6) kimeruhusu uwakilishi kutokana na ukubwa na muundo wa chama. 

KWA NINI SIJAWAHI KUPATA GAWIWO

. 

Gawiwo ni sehemu ya ziada inayopatikana baada ya hesabu za chama kukaguliwa na mkaguzi wa nje na kutoa matengo yote ya kisheria na ziada inayobaki hutolewa maamuzi na Mkutano Mkuu.

Kwa mujibu wa masharti ya chama sehemu ya 9.(e) Mgao huo hufanywa kulingana na hisa anazomiliki mwanachama, ikiwa Chama kinahitaji kukuza mtaji au kuwekeza rasilimali, kiasi hicho cha mgao kitaongezwa kwenye hisa za mwanachama, yaani zitagawiwa hisa za bonas kwa kulingana na hisa alizonazo mwanachama. Hivyo basi chama kimekuwa kikitoa gawiwo kwa kila mwanahisa na kuziongeza katika akaunti ya hisa ya kila mwanachama kwa kila mwaka wa fedha wa chama baada ya hesabu za chama kukaguliwa na kuwasilishwa katika Mkutano Mkuu.

JE NAWEZA KUCHUKUA SEHEMU YA AKIBA ZANGU?

JIBU: kwa mujibu wa sheria ya vyama vya ushirika sehemu ya viii k/f 71 (1) hairuhusu mwanachama kuchukua sehemu ya akiba yake. Kwa kuzingatia kwamba wanachama wake wanaweka akiba kwa viwango na malengo tofauti, Ushirika ukaona ni busara mwanachama aruhusiwe kuchukua sehemu ya akiba yake kwa kuacha kiwango cha Tshs 5,000/= ya kila mwezi kwenye akaunti ya mwanachama na itamlazimu atoe taarifa ya siku tisini.

KWANINI MIKOPO INACHELEWA KWA BAADHI YA WAOMBAJI.

JIBU: Katika  suala  la  utoaji wa  mikopo  chama kilishafikia azimio la  kuwa  mikopo  yote  itatoka ndani ya   muda  wa  siku saba  baada ya fomu za  mikopo kupokelewa ofisini, hata hivyo kuna baadhi ya waombaji mikopo yao huchelewa kutokana na sababu zifuatazo: –

  1. Fomu za mkopo kutotumwa kwa wakati Makao Makuu ya URA SACCOS LTD toka zilipopokelewa kwa mwakilishi wa wilaya/mkoa.
  2. Fomu kutumwa kwa kutokutumia njia isiyo rasmi, na hivyo kuchelewa kufika.
  3. Baadhi ya fomu zinatumwa zikiwa hazijakamilika/mapungufu kama vile kutokujazwa kwa usahihi, mapungufu ya viambatanisho vinavyotakiwa ambavyo ni kivuli cha kadi ya benki, salary slip halisi, nakala ya kitambulisho cha kazi,  fomu kutosainiwa na afisa mhusika ndani ya  mkoa au wilaya, fomu kujazwa kiwango kikubwa tofauti na stahili ya mwanachama.

NB: ili kuondoa mapungufu hayo, fomu zote za mikopo zipitie kwa mwakilishi wa eneo husika kwa uhakiki.

MWANACHAMA AKIFARIKI AKIWA NA MKOPO JE AKIBA/HISA ZAKE ZITAFIDIA MKOPO?

Mikopo yote inayotolewa kwa wanachama hukatiwa bima ya maisha, ambapo ikitokea mwanachama amefariki chama hakitachukua akiba/hisa wala mafao ya mifuko ya hifadhi ya jamii ya marehemu kufidia deni aliloliacha, badala yake deni hilo litafidiwa/kulipwa na mfuko wa Bima ya mkopo.

JE MNAMPANGO GANI KUONGEZA MATAWI MIKOANI

Katika mpango kazi wa Chama wa mwaka 2015- 2017 chama kimejiwekea malengo ya kujenga matawi katika baadhi ya mikoa kulingana na bajeti iliyopangwa na kupitishwa na Mkutano Mkuu, ujenzi wa matawi ni sehemu ya kipaumbele cha chama ambapo hadi sasa ujenzi umekamilika katika Kamisheni ya Polisi Zanzibar na unaendelea katika hatua za mwisho katika mikoa ya Mwanza na Tanga, vilevile ujenzi unatarajia kuanza hivi karibuni katika mikoa ya Dodoma, Mbeya na Kigoma. Lengo la ujenzi huu ni kusogeza huduma kwa wanachama, ambapo huduma zote zitolewazo Makao Makuu zitafanyika katika matawi husika.